Wednesday, February 3, 2016

Martha Nelson anogewa na muziki wa injili



MWIMBAJI wa nyimbo za injili na mcheza filamu za Bongo, Martha Nelson, ni moja ya waimbaji wa muziki huo ambao wanafanya vizuri katika tasnia hiyo kwa sasa.
Martha mama wa watoto watatu, licha ya kufanya vizuri Afrika Mashariki kwenye muziki wa injili, lakini amekuwa akipata nafasi za kuitangaza nchi katika maeneo mengine nje ya Afrika ikiwemo Ulaya na Marekani.
Mwanamama huyu anasema kwamba, muziki wa injili umekuwa ni kimbilio na kielelezo cha kumfanya atambulike kuwa ni Mtanzania popote anapokuwa anakwenda, hasa kwa sababu kazi zake zote amekuwa akitumia lugha ya Kiswahili.
Martha anasema ili kufanikiwa kwenye muziki wa injili  lazima ufuate miiko inayoongoza muziki huo nayo ni ukweli pamoja na kumshirikisha Mungu. Lakini lingine kuhakikisha kazi inayofanyika ni bora ambayo inaweza kukubalika ndani na nje Tanzania.
“Kazi ya muziki wa injili ni ngumu lakini ukimtegemea Mungu ni jambo linalowezekana kufanikiwa. Lakini kubwa kuliko yote ni kujua unatakiwa kufanya nini kwa ajili ya nani.
“Kwa mfano katika kazi yangu mpya iitwayo ‘Yupo Mungu Asiyeshindwa’ niliweza kumshirikisha Mungu kwa kiwango kikubwa naamini ndiyo sababu ya kazi hiyo kufanya vizuri kwa wakati huu.
“Naelewa kuwa si jambo rahisi lakini niseme kwamba muziki huu bado unahitaji nguvu ya ziada kuhakikisha unakuwa na kupaa zaidi ya ilivyo sasa kwa sababu inawezekana kwani tunayemtumikia ni mkuu zaidi ya yeyote,” anasema Martha.
Mwimbaji huyo anasema katika kazi hiyo mpya ina jumla ya nyimbo nane ambapo kwa sasa imeshatoka ingawa sokoni itaingia katikati ya Februari. Baadhi ya nyimbo zilizozopo kwenye albamu hiyo ni pamoja na Usifiwe Jehova, Amenitoa Mbali, Acheni Niimbe na nyingine nyingi.
“Kazi hii natarajia itaingia sokoni katikati ya Februari ili mashabiki wangu waweze kuniunga mkono, ingawa kubwa kuliko yote ni kuhakikisha ujumbe wangu wa Neno la Mungu unawafikia watu wote.
Hii ni albamu ya pili kwa Martha ambapo ya kwanza aliitoa miaka mitano iliyopita iliyokwenda kwa jina la Unawaza Nini.
“Baada ya kutoa albamu yangu ya kwanza nilikaa zaidi ya miaka miwili nikiandaa kazi mpya, lakini baadaye nilikaa tena miaka hadi kuingia studio na kurekodi video. Kwa lugha rahisi ni kwamba, kazi hii nimeifanya kwa muda wa miaka mitano.
“Sababu kubwa zilizonifanya kuamua kuchukua muda mrefu katika kazi moja ni kutokana na kutafuta ubora, unapotaka kufanya kitu bora lazima ufanye kwa umakini lakini kitu chenye uhakika, mimi nilifanya hivyo kwa kuamini kwamba ninaweza kufanya kitu bora hasa ikizingatiwa kuwa hii ni kazi ya Mungu lazima iwe bora,” alisisitiza nyota huyo.
Mbali na kufanya vizuri kwenye muziki, lakini katika tasnia ya filamu amefanya kazi nyingi ikiwemo Poster Shadow, Haki, Tutafika pamoja na nyingine nyingi. Juu ya sekta hiyo, Martha ameishauri Serikali kuhakikisha kuwa inaisimamia sekta ya filamu vizuri pamoja na sanaa kwa ujumla ili kuzalisha ajira nyingi zaidi.
“Tunahitaji sanaa iwe ni kazi rasmi ambayo inaweza kusimamia maendeleo ya uchumi kikamilifu. Naamini kuwa kwa kutumia njia hii itasaidia katika mapambano dhidi ya umasikini,” amesisitiza mkali huyo wa injili. 

Martha Nelson katika picha mbalimbali.