Saturday, August 16, 2014

Man United kuzoa pointi 18 za fastafasta





NA EZEKIEL TENDWA
LIGI Kuu ya England inatarajiwa kuanza rasmi mwishoni mwa wiki ijayo ambapo nyasi za viwanja mbalimbali zitawaka moto kila timu ikihitaji kujikusanyia pointi za mapema mapema kabla ligi yenye haijachanganya.

Timu zote zimekuwa zikifanya maandalizi ya nguvu kwa ajili ya kuhakikisha wanafanya vizuri wengine wakitaka kuchukua ubingwa na wengine kuepuka mkasi wa kushuka daraja kwani katika soka kila mmoja ana malengo yake.

Katika ratiba iliyotolewa na chama cha soka nchini humo FA, inaonekana kuwabeba Manchester United katika michezo yao sita ambapo kama wataingia na moto waliouonyesha nchini Marekani kwenye mechi za kujiandaa na ligi hiyo, ambapo kama mwendo utakuwa huo huo watajikuta wakikusanya pointi 18 za mapema bila kikwazo chochote.

Wakiwa nchini Marekani mabingwa hao wa zamani wa  England waliwatoa nishai vigogo kama Los Angeles Galaxya Marekani, AS Roma na Inta Milan zote zinazoshiriki Ligi Kuu ya Italia, Real Madrid ya Hispania pamoja na Liverpool ya England.

Kikosi hicho ambacho kipo chini ya kocha wao mpya Louis Van Gaal kitaanza mchezo wao wa kwanza Jumamosi ya wiki ijayo dhidi ya Swansea, licha ya wapinzani wao kuwa katika kiwango kizuri lakini uwezo wa kutoa upinzani kwa Mashetani Wekundu  hao ni mdogo ingawa kwenye soka lolote linaweza kutokea.

Mchezo wa pili kwa Van Gaal na kikosi chake itakuwa dhidi ya Sunderland uwanja wa ugenini ambapo katika msimu uliopita Sunderland licha ya kuwatoa kijasho Man United lakini historia inaweza ikaendelea kuwabeba Man United.

Agosti 30 Man United, watakuwa tena ugenini kukipiga na Burnley FC ukiwa mchezo wa tatu ambapo kutokana na ari ya ushindi waliyonayo watataka kuondoka na pointi ili tu kujiwekea mazingira mazuri ya kuhakikisha wanatafuta nafasi ya kushiriki michuano ya UEFA.

Wakati Arsenal wakiwa na kibarua cha kuwakabili mabingwa watetezi wa michuano hiyo Manchester City katika uwanja wao wa Emirates Septemba 13, kwa upande wao Man United wataendelea kujitafutia pointi nyingine katika uwanja wao wa Old Trafford dhidi ya QPR Septemba 14.

Van Gaal atakuwa tena na kibarua cha kutafuta pointi kwa timu ndogo ya Leicester ugenini Septemba 20 kabla ya kumalizia kubarua cha kucheza na dhidi ya West Ham Septemba 27 kwenye uwanja huo huo wa jijini Manchester.

Hiyo ndiyo michezo sita ambayo kwa vyovyote Manchester United watatakiwa kutafuta pointi 18 kabla ya kuanza kukwaana na vigogo ambapo baada ya michezo hiyo watavaana na wabishi Everton kabla ya kupata mteremko mwingine dhidi ya West Bromwich Albion na baadaye kuja kucheza na Chelsea 0ktoba 26.

Arsenal wao wataanza kwa mteremko kidogo mchezo wa kwanza watakapocheza na Crystal Palace na baadae kukutana na wabishi Everton ugenini huku Manchester City wao wakianza na wagumu Newcastle kabla ya kuwavaa Liverpool.

Timu hizi kubwa za Manchester United, Manchester City, Liverpool, Arsenal, pamoja na Chelsea ndizo zinazotafuta nafasi nne za kwanza ili kupata tiketi ya kushiriki UEFA ambapo msimu huu Manchester United wamepigwa kumbo baada ya kumaliza wakiwa nafasi ya saba msimu uliopita.

Kwa maana hiyo ni kwamba msimu ujao Ligi Kuu England itakuwa moto wa kuotea mbali kwani timu hizi vigogo moja lazima iwapishe wenzake kwani sheria inaruhusu timu nne tu kutinga kwenye michuano hiyo ya UEFA inayoheshimika duniani kote.

No comments:

Post a Comment