Friday, November 21, 2014

Sikinde, Kopa kuwasha moto Swahili Arts Carnival



NA MWANDISHI WETU
BENDI Kongwe ya muziki wa dansi, Sikinde pamoja na Malkia wa muziki wa Taarab Afrika Mashariki, Khadija Kopa ni miongoni mwa wanamuziki watakatoa burudani kwenye Tamasha la Sanaa na Ubunifu wa Mswahili (Swahili Arts and Creative Carnival).
Akizungumza na mtandao wa jamii,  mmoja wa waratibu wa tamasha hilo, Ahadi Kakore amesema kuwa Sikinde ni miongoni mwa bendi zinazopiga muziki wa Kiswahili asilia ndiyo maana wameamua kuiweka kuwa bendi rasmi ya dansi ya tamasha hilo.
Aliongeza kuwa kwa upande wa Khadija Kopa naye atakuwa na bendi yake ya Ogopa Kopa Classic ambayo siku hiyo imeahidi kuimba nyimbo zake mpya ambazo nyingi zitaimbwa kwa mara ya kwanza siku hiyo.
“Mbali ya kuwepo kwa burudani hizo za muziki lakini haina maana kuwa ndiyo tumefunga mlango kwamba hatutakuwa na wasanii wengine ila bado tupo kwenye mazungumzo na wanamuziki nyota wa kizazi kipya kwani tumelenga kuwafikia watu wa rika zote.
“Pamoja na burudani za watu wazima pia watoto nao hawajaachwa nyuma kwa sababu kutakuwa na michezo maalum kwa watoto na zawadi nyingi zipo kwa ajili yao ili kuhakikisha wanafurahia siku hiyo.
Mbali na muziki, burudani nyingine zitakazokuwepo siku hiyo ni maonyesho ya filamu za Kiswahili, maonyesho ya mavazi, vyakula, nyama choma, vinywaji pamoja na michezo ya watoto na maonyesho ya bidhaa za wajasiriamali na watu 1,000 wa kwanza watapata zawadi langoni,” alisema Kakore.
Swahili Arts and Creative Carnival linatarajiwa litafanyika Novemba 29 mwaka huu kwenye viwanja vya Posta, Kijitonyama jijini Dar es Salaam huku likiwalenga watu wazima na watoto kuanzia saa 4:00 asubihi hadi usiku wa manane.
Tamasha hilo limeandaliwa na Kampuni ya Swahili Arts & Creative Carnival kwa kushirikiana na Hildelly Solution na Wazalendo Bright Media kwa udhamini wa Amo Transport Solutions, Coca Cola, Tigo, Oriflem, Chibuku, Global Publishers, CTN na Sibuka TV. 

No comments:

Post a Comment