Thursday, July 17, 2014

Wazari makala anusurika kupigwa


Naibu Waziri wa Maji, Amos Makalla, jana aliondolewa chini ya ulinzi mkali wa polisi katika mkutano wa hadhara baada ya kuzuka vurugu zilizotokana na wafuasi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), jijini Dar es Salaam.

Vurugu hizo zilizodumu kwa takriban dakika 30, zilitokana na Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Kinondoni, Salum Madenge, kusalimia wananchi katika mkutano huo, kitendo ambacho kilionekana kutowapendeza wafuasi wa Chadema kwa madai kuwa haukuwa mkutano wa CCM.

Tukio hilo lilitokea jana katika uwanja wa Goba, jijini Dar es Salaam, wakati Makalla alipowasili na viongozi mbalimbali kutoka wizara hiyo pamoja na viongozi wa CCM na Chadema kwa ajili ya kuzungumza na wananchi wa kata hiyo kuhusiana na tatizo la maji na namna serikali ilivyojipanga kutatua kero hiyo.

Kitendo cha mwenyekiti huyo wa CCM kusimama na kusalimia wananchi hao, kiliwafanya wafuasi wa Chadema kulipuka na kuanza kuvamia uwanja wakimtaka aondoke. Wafuasi hao wa Chadema walisema mkutano haukuwa wa CCM na kwamba, walichokuwa wakikitaka ni maji na siyo viongozi wa CCM kuzungumzia ilani zao.

Kitendo hicho kiliwafanya wafuasi wa CCM nao kuanza kupiga kelele za kuwataka viongozi wa Chadema waliokuwa wamekaa jukwaa kuu kuondoka ili kuwapo na usawa.

Kutokana na kelele za wafuasi hao kukithiri, askari polisi waliokuwapo walilazimika kutumia nguvu za ziada kuwadhibiti wafuasi hao.
Polisi waliwazingira viongozi waliokuwa jukwaa kuu kulinda usalama wao uliokuwa umetishiwa na wafuasi wa vyama hivyo.

Hata hivyo, juhudi za polisi hazikufua dafu kwani vurugu ziliongezeka na hivyo kuwalazimu kumuondoa jukwaani Makalla na kumuingiza kwenye gari lake, huku viongozi wa Chadema wakiendelea kuzozana na polisi.

Akizungumza na waandishi wa habari baada ya kuondolewa jukwaani akiwa ndani ya gari lake, Makalla alisema vurugu hizo zimesababisha wananchi wakose haki yao ya msingi kwa sababu siasa zimeingilia kati mkutano huo.

“Haya niliyatarajia. Kwa hiyo, siwezi kushangaa wakati wananchi wengine wakiwa wanafurahia ujio wa waziri katika maeneo yao watoe malalamiko yao, hali imekuwa ya kisiasa zaidi na matokeo yake tumeshindwa kuzungumza na wananchi mambo ya msingi,” alisema Makalla.

Alisema amekamilisha jukumu lake kwa kufika kwa wananchi ili awaeleze mipango ya serikali ya kutatua kero ya maji, lakini mkutano umeingiliwa na wanasiasa wasio wakazi wa kata hiyo.

Kwa upande wake, Mbunge wa Ubungo (Chadema), John Mnyika, alisema vurugu hizo zimetokana na wafuasi wa CCM, ambao siyo wakazi wa eneo hilo kuingilia kati ili Makalla asizungumze na wananchi.

“Kitendo cha Makalla kuondoka na kuacha wananchi wakiwa hapa, huku wanachama wake wakiendelea kufanya vurugu ni wazi kuwa anakwepa kujibu maswali ya wananchi kuhusu masuala ya maji. Hivyo, sisi hatutaondoka mpaka wanachama wetu wafahamu ni lini watapata maji,” alisema Mnyika.

Awali, Makalla na Mnyika walitembelea maeneo ya Kigogo na kuwakamata watuhumiwa watano wa wizi wa maji, ambao walikuwa wamejiunganishia maji kinyemela.

Akizungumza baada ya kufanya ukaguzi katika nyumba hizo, Makalla alisema viongozi na wananchi wana majukumu ya kuwatambua na kuwaripoti watu, ambao wanahujumu uchumi wa nchi.

Alisema watu watano waliokamatwa wanaikosesha Dawasco mapato aliyodai ni Sh. bilioni 1.2 kwa mwezi.

“Hawa, ambao wamekamatwa leo, lazima wafikishwe katika vyombo vya dola ili kuchukuliwa hatua za kisheria, ikiwamo kuwagawia wananchi maji yote waliyoyahifadhi katika matanki yao, pamoja na mali zao kuwa chini ya ulinzi wakati sheria inachukua mkondo wake,” alisema Makalla.

Makalla alianza ziara juzi katika jiji la Dar es Salaam kukagua miundombinu ya maji pamoja na kuzungumza na wananchi kuhusiana na kero za maji na namna serikali ilivyojipanga kumaliza tatizo hilo.

HABARI NA MARY GEOFREY 
CHANZO - NIPASHE

No comments:

Post a Comment