Tuesday, October 28, 2014

Yanga yafanya umafia Bukoba




 JUMA KASESA NA EZEKIEL TENDWA
YANGA SC imeifanyia umafia Kagera Sugar kwa kutanguliza kikosi kazi maalumu kwenda kuichunguza timu hiyo, kabla ya mchezo wao na timu hiyo Jumamosi wiki hii kwenye Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba.
Kikosi cha kocha Mbrazil Marcio Maximo kinataka kuendeleza wimbi la ushindi ili kutimiza dhamira yao ya kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu unaoshikiliwa na Azam FC.
Kwa kutambua Kagera ni wagumu kufungika nyumbani, Yanga imefanya tena kile ilichokifanya msimu uliopita kwa kutuma kikosi kazi maalumu cha kuichunguza timu hiyo mbinu zake ili kurahisisha mipango yao ya kuondoka na pointi tatu Uwanja wa Kaitaba.
Msimu uliopita Yanga ilituma jopo la matajiri wakiongozwa na Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya klabu hiyo, Stanley Katabaro ambaye ana asili ya Mkoa wa Kagera na baadhi ya wajumbe wenzake wa Kamati ya Utendaji kwenda kuichunguza timu hiyo na kuwasilisha taarifa muhimu kwa benchi la ufundi wakati huo likiwa chini ya kocha Fred Felix Minziro 'Majeshi'.
Na safari hii Yanga imetuma jopo la watu maalumu wa benchi la ufundi kwenda Wilaya ya Misenyi, ambako Kagera Sugar imejichimbia ikijifua chini ya kocha wake, Jackson Mayanja tayari kwa mchezo huo ambao ni gumzo kwa sasa.
Habari za uhakika kutoka ndani ya uongozi wa Yanga zimelieleza DIMBA Jumatano kwamba, jopo hilo limeshaingia Misenyi likiwachunguza wachezaji wa Kagera na limekuwa likiwasilisha taarifa kwa benchi la ufundi kila inapomalizika programu ya mazoezi ya timu hiyo.
Aidha, imeelezwa kikosi kazi hicho kilichopelekwa si rahisi kugundulika kwani Yanga imebaini ingempeleka tena Katabaro safari hii ingeweza kushtukiwa mpango wake mapema na Kagera.
Itakumbukwa Yanga ilikuwa haijapata ushindi uwanja huo tangu mwaka 2011 kabla ya kuvunja mwiko huo Oktoba 12, 2013 kwa kuichapa Kagera Sugar mabao 2-1.
Shukrani kwa mabao ya Mrisho Ngassa dakika ya 2 na Hamis Kiiza 'Diego' dk 60, yaliyoiwezesha timu hiyo kuondoka na ushindi kwenye uwanja huo.
Kikosi cha Yanga kimejichimbia Kahama kabla ya kuelekea Bukoba ambapo leo kinatarajiwa kucheza mchezo wa kujipima nguvu dhidi ya Ambassador FC ya mjini humo.
Maximo ameupania mchezo huo na ndio maana ameamua kusafiri na kikosi chake chote cha wachezaji 28 ambapo jana walijifua kikamilifu kuhakikisha wanarudi Dar es Salaam na ushindi mnono kutoka kwa wakata miwa hao wa Kagera.
Kikosi cha Maximo kitaingia kwenye mchezo huo kikiwa na kumbukumbu nzuri ya ushindi mnono wa mabao 3-0 iliyoupata kwa Stand United mwishoni mwa wiki iliyopita wakati Kagera wao watakuwa na hasira ya kulazimishwa sare 1-1 nyumbani na 'Wagosi wa Kaya' Coastal Union.
Maximo amesema kwa sasa akili yake yote ni kuhakikisha hadondoshi pointi hata moja iwe ni Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam au viwanja vya mikoani yote hayo ikiwa ni kutimiza ahadi ya kuipa Yanga ubingwa.
Kocha huyo anajivunia kikosi kilichokamilika kila idara kuanzia golini hadi safu ya ushambuliaji ambapo hayo yote yalijidhihirisha katika mtanange dhidi ya Stand United walipopata ushindi mnono wa mabao 3-0 ambayo tangu ligi ianze msimu huu hawajawahi kuyafunga.
Jeuri kubwa aliyonayo Maximo ni kurudi kwa kiwango cha mshambuliaji wa timu hiyo, Jerryson Tegete alipofunga mabao mawili kwenye ushindi huo dhidi ya Stand huku lingine likifungwa na Mbrazil Geilson Santos ‘Jaja’.
Kazi kubwa iliyopo kwa Maximo ambayo inamfanya akune kichwa ni namna ya kuamua nani amuanzishe kikosi cha kwanza na nani abaki hasa kwenye safu ya ushambuliaji huku viungo nao wakipigana vikumbo kwa kuonyesha uwezo mkubwa.
Kutokana na kazi kubwa iliyoonyeshwa na Tegete kwa kufunga mabao mawili ni dhahiri kazi itakuwa kubwa kwa Jaja kuhakikisha anatetea nafasi yake hiyo ambapo pia Husein Javu pamoja na Nizar Khalfani nao wanakuja juu.
Kwa sasa kwenye kikosi cha Yanga, Tegete ndiye anayeongoza katika suala zima la upachikaji wa mabao mawili licha ya kwamba amecheza kwa dakika chache katika mchezo mmoja dhidi ya Stand United huku michezo yote minne akisugulishwa benchi.
Yanga wapo nafasi ya tatu wakiwa na pointi 10 sawa na Azam FC iliyopo nafasi ya pili huku Mtibwa Sugar wakiwa kileleni baada ya kujikusanyia pointi 13 timu zote zikiwa zimecheza mechi tano.
Kwa upande wao Kagera Sugar ambao watakuwa uwanja wao wa nyumbani kuwakabili Yanga, wapo katika nafasi ya saba na pointi sita ambapo mchezo wao huo unatabiriwa kuwa mkali kila timu ikihitaji kusogea mbele.

No comments:

Post a Comment