Tuesday, October 28, 2014

Phiri apata nguvu mpya



NA JIMMY CHIKA
KOCHA wa Simba Mzambia, Patrick Phiri amefumba macho baada ya uongozi wa klabu hiyo kuwapiga chini nyota watatu wa timu hiyo, akapiga ngumi kifuani na kusema kikosi chake sasa kitazaliwa upya.
Phiri amesema uamuzi huo umerudisha ari yake ya kukinoa kikosi hicho kwani kabla ya hapo alionekana kukata tamaa.
Jana kocha huyo alikataa kufafanua juu ya tishio la Kamati ya Utendaji ya Simba iliyoketi mkoani Iringa na kutoa maamuzi ya kuwatimua wachezaji wake watatu, Shaaban Kisiga, Haruna Chonongo na Amri Kiemba, lakini akasema mabadiliko yaliyofanyika anaamini yataleta taswira mpya.
Akizungumza na gazeti hili, Phiri alisema yeye kama kocha aliwaambia viongozi wakae na kuangalia tatizo liko wapi na walirekebishe kwa hiyo anaamini kama waliona tatizo liko kwa wachezaji hao basi  wametekeleza maagizo yake.
Hata hivyo, mabadiliko hayo hayakupokewa vizuri na mashabiki wa Simba ambapo jana baadhi yao walivamia makao ya klabu hiyo na kuendesha vikao visivyo rasmi kupinga hatua hiyo.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti mashabiki hao walisema, kinachoigharimu Simba kwa sasa ni hali ya kutokuwepo kwa uhusiano mzuri baina yao na kamwe si wachezaji.
Mashabiki hao wamewatetea wachezaji hao ambao wote hucheza nafasi ya kiungo, kuwa watahitajika sana katika mechi zijazo hasa kutokana na uzoefu wao.
Kiemba ambaye ndiye pekee aliyeongelea suala la kutimuliwa kwao, alisisitiza kwamba amepoteza ari ya kuitumikia timu hiyo kufuatia kitendo hicho alichokiita ni udhalilishaji kwake.
Rais wa klabu hiyo, Evance Aveva alitaja sababu ya kutimuliwa Kiemba kuwa ni kushuka kiwango, huku Kisiga na Chonongo wakituhumiwa kwa utovu wa nidhamu.
Hata hivyo, Aveva aliliambia DIMBA kwamba, wachezaji hao bado wako chini ya klabu hiyo hadi pale kikao cha kuwajadili kitakapofanyika keshokutwa Ijumaa na kutoa maamuzi ya pamoja.
Wakati hali ikiwa hivyo, uongozi wa Simba umempa Phiri mechi mbili zijazo za kushinda, dhidi ya Mtibwa Sugar Jumamosi hii na Ruvu Shooting wiki ijayo, vinginevyo utavunja mkataba wake.
Phiri amepewa mechi hizo ili kuinasua timu hiyo kutoka dimbwi la sare ambalo limeiandama timu hiyo tangu kuanza kwa ligi.
Katibu Mkuu wa Simba, Stephen Ally aliwaambia waandishi wa habari jana makao makuu ya klabu hiyo Mtaa wa Msimbazi kuwa, Phiri anaweza kuondolewa baada ya mechi hizo mbili iwapo matokeo hayatakuwa mazuri.
Ally amesema kwamba, sababu ya Kamati ya Utendaji kufikia maamuzi hayo ni kwamba, wakati anaajiriwa Agosti mwaka huu, Phiri alipewa kila alichokihitaji ili kujenga timu.
"Alitaka kambi ya Zanzibar akapewa, akataka mechi za majaribio akapatiwa na timu imeendelea kuwa kambini muda wote wa mashindano, ikiwemo ya Afrika Kusini," alisema Ally.
Phiri alifanya vizuri katika mechi za kirafiki, lakini baada ya kuanza kwa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzaia Bara ametoa sare mechi zote tano na Jumamosi wiki hii atakuwa Uwanja wa Jamhuri dhidi ya vinara, Mtibwa Sugar.
Aidha, Katibu huyo amesema kwamba wachezaji watatu waliosimamishwa, Kisiga, Amri Kiemba na Haroun Chanongo watakutana na Kamati ya Nidhamu Ijumaa kujibu tuhuma zao.
Katika hatua nyingine mechi ya Simba na Mtibwa inazidi kuwa katika mazingira magumu kwa timu hiyo ya Msimbazi hasa ikizingatiwa kwamba wachezaji wengine nao wamepewa sharti la kushinda mechi hiyo ili kuepuka adhabu kama iliyowakumba wenzao.
Wakizungumza kwa masharti ya kutotajwa majina yao, baadhi ya wachezaji wameelezea kuihofia mechi hiyo kuliko ilivyokuwa ile iliyowakutanisha na Yanga, iliyopigwa Oktoba 18 kwenye Uwanja wa Taifa na kumalizika kwa matokeo ya suluhu 0-0.
Kwa upande wao uongozi wa Mtibwa Sugar umewataka wenzao wa Simba kutumia busara kumaliza matatizo yao lakini wasiuchukulie mchezo wao kama kigezo cha kutimua wachezaji.
Kocha wa Mtibwa, Mecky Mexime aliliambia DIMBA kwamba, maandalizi yao na nia ya kutwaa ubingwa msimu huu ndiyo iliyowafikisha hapo na kwamba wana uhakika wa kushinda mechi yao dhidi ya Simba itakayopigwa kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro.
  Emmanuel Okwi (jezi nyekundu), mmoja wa wachezaji tegeemo kwa kikosi cha Patrick Phiri.

No comments:

Post a Comment