Thursday, December 24, 2015

Yanga yapeleka majina 24 CAF




NA SAADA SALIM
KOCHA Mkuu wa Yanga Mholanzi, Hans Pluijm, ana hasira za msimu uliopita kushindwa kuifikisha timu hiyo pazuri kwenye michuano ya kimataifa lakini safari hii ameapa lazima kieleweke.
Unajua kwanini? Mholanzi huyo safari hii amepeleka Shirikisho la Soka Barani Afrika (CAF), majina ya silaha zake 24 huku 10 zikiwa za kimataifa tayari kwa kufanya makubwa mapema Februari mwakani kwenye michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika.
Katika majina hayo 24 ukiwaacha, Thaban Kamusoko, Donald Ngoma, Amissi Tambwe, Haruna Niyonzima, Issoufou Boubacar Garba, Vicent Bossou na Mbuyu Twite, Pluijm ameamua kuleta majembe mengine mawili ya kimataifa ingawa tayari inaye mchezaji mmoja Mnyarwanda, Jerome Sina, anayefanyiwa majaribio.
DIMBA Jumatano limethibitishiwa kwamba Yanga itawaleta straika, Spencer Sautu kutoka Ashanti Gold ya Ghana, ambaye ataungana na beki shupavu aitwae Kabongo kutoka Congo (DRC).
Wawili hao wanakuja wakati wowote nchini kuanzia sasa kufanya majaribio ingawa inaelezwa kwamba kocha Hans anavifahamu vyema viwango vyao vya soka.
Chanzo cha habari cha uhakika kimelieleza gazeti hili kuwa ujio wa wawili hao utafanya timu hiyo iwe na wachezaji 10 wa kimataifa ili kukifanya kikosi chao kiweze kuhimili vishindo vya michuano hiyo mikubwa zaidi barani Afrika na yenye utajiri mkubwa inayoandaliwa na CAF.
Aidha, chanzo hicho kilieleza kuwa Yanga bado inaendelea kumfanyia majaribio kiungo wa Rayon Sport, Jerome Sina, ingawa usajili wake utasubiri kwanza ili kulinganishwa kiwango na Sautu.
Jerome mwenye miaka 26 raia wa Congo (DRC) amemvutia Pluijm na inaelezwa iwapo atafuzu majaribio atasajiliwa mwishoni mwa msimu kwa ajili ya kuibeba Yanga.
"Sasa hivi hatutaki masihara kwani tunahitaji kufika mbali zaidi, ukiangalia msimu uliopita hatukufikia malengo yetu kwa vile tulitolewa mapema ndiyo maana usajili wa wachezaji wa kigeni unafanyika kwa umakini mkubwa tukiamini watasaidiana vyema na wazawa ili mwakani tuweze kuvunja rekodi yetu," alisema mtoa habari.
Alisema tayari benchi la ufundi la timu hiyo limependekeza kupeleka idadi ya majina 24 kwa ajili ya michuano hiyo ya kimataifa ambapo wachezaji hao wawili wanaotarajia kutua hapa nchini wataungana na Sina kwa ajili ya majaribio na baadaye kusaini.
Katika hatua nyingine, Yanga imebadilisha mipango yake ya kwenda kujifua nchini Ghana kwa ajili ya kujiandaa na michuano hiyo na badala yake watabaki hapa nchini na kuzialika timu za nje ili kucheza nazo mechi za kujipima.
Kocha wa Yanga, Hans Van Der Pluijm, ameliambia DIMBA Jumatano kuwa wana mpango wa kuzialika timu tatu za kimataifa ambazo ni Ashanti Gold ya Ghana pamoja na Gor Mahia na KCB zote za Kenya.
"Mpango wetu wa kwenda nje ya nchi umekufa kutokana na ratiba kuingiliana, lakini tumezialika timu nne ambapo mbili za KCB na Gor Mahia tayari zimethibitisha huku Ashanti ikiwa bado," alisema kocha huyo.

No comments:

Post a Comment