Friday, July 11, 2014

Nooj: Stars itaichinja Mambas



KOCHA Mkuu wa timu ya Taifa, Taifa Stars,  Mart Nooj amesema kuwa kikosi chake kipo vizuri na kitaweza kushinda mchezo wa kufuzu Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) mwakani nchini Morocco dhidi ya Msumbiji ‘Mambas’. 
Nooj alisema kuwa timu inatarajiwa kuondoka leo jijini kwenda kuweka kambi nyingine Tukuyu, mkoani Mbeya ambapo itarejea siku tatu kabla ya mechi.

Akizungumzia kambi ya Botswana alisema, ilikuwa nzuri na imesaidia kuwajenga kutokana na kufanya mazoezi na kupata mechi tatu za kujipima nguvu.
Amesema katika mechi hizo, walifungwa mbili, moja dhidi ya timu ya taifa ya Botswana mabao 4-2 na nyingine dhidi ya timu ya Jeshi la nchini humo, BDF walishinda moja 3-1 na kufungwa moja 2-1.

Katika hatua nyingine wachezaji wawili wa timu hiyo Jonas Mkude na Himid Mao ni majeruhi ambapo Daktari wa timu hiyo Bile Haonga alisema kwamba  wamefanyiwa vipimo na wanaendelea na uangalizi.

Kwa upande wake nahodha wa timu hiyo Nadir Haroub ‘Cannavaro’ alisema kuwa wamejifunza mengi katika kambi ya Botswana, na kufungwa kwao mechi mbili kati ya tatu walizocheza ni uzembe  kwenye safu ya ulinzi.

“Kikubwa ni Watanzania kuendelea kutuunga mkono maana mpira unabadilika na tunajua kama tuna kazi kubwa katika mechi dhidi ya Msumbiji,” alisema Canavaro ambaye pia ni nahodha wa Yanga.
Stars na Msumbiji zinatarajiwa kukutana Julai 20 mwaka huu, kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam ambapo timu hiyo, imerejea mwishoni mwa wiki iliyopita ikitokea Botswana kwa kambi ya wiki mbili.

NA SALMA JUMA

No comments:

Post a Comment