Monday, November 3, 2014

sera ya elimu kufutwa

Serikali imesema wakati wowote kuanzia sasa, itaifuta sera ya elimu inayotumika nchini kutokana na kukamilika kwa mchakato wa uanzishwaji sera mpya ambayo imepangwa kuzinduliwa na Rais Jakaya Kikwete, mwezi huu.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Profesa Sifuni Mchome, alisema sera hiyo tayari imepitishwa baada ya kujadiliwa na vikao vya Baraza la Mawaziri.

Akizungumza jana katika uzinduzi wa Chuo Kikuu kipya cha  Mwenge (MWECAU) kinachomilikiwa na Kanisa Katoliki kilichopo nje kidogo ya mji wa Moshi, Profesa Mchome alisema uamuzi huo wa Wizara hiyo umelenga kuhakikisha kwamba sekta hiyo inakua na kukidhi mahitaji na matarajio ya jamii ndani na nje ya nchi.

“Tumeanza kuboresha elimu yetu kwa kuangalia eneo la mifumo ya kisera na kimsingi, tumefumua sera inayotumika. Huko tumeangalia mwelekeo wa sasa wa dunia inavyokwenda, mabadiliko ya sayansi na teknolojia, viwango na vigezo vya ubora wa elimu inayotolewa,” alisema.

Alisema mambo mengine yaliyohakikiwa wakati wa uandaaji wa sera mpya ni njia za kuwapata wahitimu wenye elimu bora na yenye viwango ambavyo vimebainishwa na kuwekwa kisera ili kuepusha mambo ya kufikiri au kubuni.

Aliyataja mengine yaliyoangaliwa na kuchambuliwa na jopo la wasomi kuwa ni namna taifa litakavyosimamia elimu yake kwa ufanisi katika ngazi za chini, wilaya mikoa na Taifa.

”Jambo jingine lililoangaliwa kisera ni namna tutakavyoiweka mitaala ya elimu iweze kutufikisha kwenye malengo ambayo ifikapo mwaka 2025 Tanzania itakuwa ni taifa lililosheheni watu

wa kipato cha kati ambacho kina wananchi wanaofahamu, wenye elimu, ujuzi, uwezo wa kupambanua na kuzikabili changamoto za maisha na ajira,” alisema.

Hata hivyo, Askofu wa Jimbo Katoliki la Moshi, Isack Amani, akizungumza kwenye mahafali ya saba ya chuo hicho, alisema sekta ya elimu inahitaji mabadiliko makubwa kwa kuwa baadhi ya wasomi na wanafunzi hivi sasa wengi wao hawamudu kutekeleza majukumu yao kutokana na kutegemea akili zao zisukumwe na nguvu ya kilevi.

Chuo Kikuu cha Mwenge kimepandishwa hadhi kuwa Chuo Kikuu baada ya kujiengua katika mwavuli wa vyuo vingine 12 vishiriki vya Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustino (SAUT)

CHANZO chingaone.com

No comments:

Post a Comment