Tuesday, February 3, 2015

Simba yafuata dawa Zanzibar

SAADA AKIDA NA SALMA MPELI

KOCHA wa Simba, Goran Kopunovic, ameziangalia silaha zote ndani ya kikosi chake kinachoshiriki Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara kuuomba uongozi umpe muda zaidi ajichimbie na timu kisiwani Zanzibar kwa ajili ya kukipika zaidi kikosi chake.

Goran anaonekana kunogewa na marashi ya Zanzibar yaliyompa ubingwa Kombe la Mapinduzi na ndiyo maana ameamua kukipeleka tena kikosi chake kisiwani humo kwa ajili ya maandalizi ya mechi za mzunguko wa pili wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.
Simba imekuwa na desturi ya kujichimbia kisiwani humo, hasa inapokabiliwa na mechi ngumu pekee, ikiwemo ya mahasimu wa jadi kisoka, Yanga, lakini sasa Kopunovic amesema kambi ya Zanzibar ndiyo anaamini itampa ubingwa.
Mserbia huyo alianza kazi ya kuinoa Simba Januari Mosi, mwaka huu, kwenye michuano ya Mapinduzi na kuipa taji hilo, akisifia mazingira ya utulivu yalisaidia timu yake kufanya vema.
Habari za uhakika kutoka ndani ya uongozi wa Simba zinaeleza Kopunovic amependekeza timu yake kurejea visiwani Unguja baada ya kupaona ni sehemu tulivu kwake kuweza kuwajenga wachezaji kisaikolojia.
"Unajua kule ndipo alipoanzia kazi, kwani aliikuta timu katika michuano ya Mapinduzi ambapo ameyapenda mazingira ya kule akidai ni sehemu tulivu, hivyo ameuomba uongozi kuhakikisha unawafanyia mpango ili timu iweze kwenda tena kujichimbia huko," kilisema chanzo hicho.
Kwa mujibu wa chanzo hicho, timu hiyo itakwenda kisiwani humo baada ya mchezo wao wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara dhidi ya Coastal Union, utakaopigwa mwishoni mwa wiki hii katika Uwanja wa Mkwakwani, jijini Tanga.
DIMBA Jumatano lilimtafuta Ofisa Habari wa klabu hiyo, Humphrey Nyasio ili kuzungumzia suala hilo, ambapo hakukubali wala kukataa zaidi ya kusema akili yao yote ipo katika mchezo wao huo dhidi ya Coastal Union, kwani wanahitaji pointi zote tatu.
Akizungumzia kurejea kwa kipa wao namba mbili, Hussein Sharrif 'Cassilas', alisema mwishoni mwa wiki hii anatarajiwa kuungana na wenzake katika mazoezi mara baada ya kumaliza mchezo wao dhidi ya Coastal Union.
"Cassillas tunatarajia atajiunga na wenzake mwishoni mwa wiki hii baada ya kutoka Tanga, suala la beki wa kati, Joseph Owino bado anaendelea na matibabu, kwani aliumia nyonga," alisema Nyasio.

Baadhi ya wachezaji wa Simba wakiwa wanaingia uwanjani.

No comments:

Post a Comment